Thursday, December 14, 2017

TANZANIA YAOMBA UMOJA WA MATAIFA KUFUATILIA KWA KINA VIFO VYA WANAJESHI WETU


Tanzania imeutaka Umoja wa Mataifa UN kufanya uchunguzi wa kina na huru kuhusu chanzo cha tukio la shambulio la waasi wa kundi la ADF lililosababisha vifo vya wanajeshi 14 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania JWTZ waliokuwa wakilinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo,DRC.
Akizungumza kwenye shughuli ya kuaga miili ya wanajeshi hao iliyofanyika katika viwanja vya makao makuu ya JWTZ Upanga,Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kasim Majaliwa amesema Umoja wa Mataifa unapaswa kuchunguza tukio hilo na kwamba serikali ya Tanzania inaamini uchunguzi huo utaanza hivi karibuni
"Japo matukio kama haya hutegemewa na hutokea,lakini hatujawahi kupoteza wapiganaji wengi na kwa mpigo kama hivi”.Amesema Waziri Mkuu Majaliwa

Hata hivyo Waziri Mkuu Majaliwa amewataka wanajeshi wa Tanzania wanaolinda amani nchini DRC wasirudi nyuma au kukatishwa na tukio hilo badala yake amewaasa kuchukua tahadhari zaidi.

Akizungumza kwenye shughuli hiyo,Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dk. Hussein Mwinyi amesema wanajeshi waliouawa ni mashujaa wa Taifa na kuondoka kwao kumeacha pengo kubwa katika Taifa.
Dkt. Mwinyi amesema “Kuondoka kwa wanajeshi hawa kusiturudishe nyuma katika majukumu yetu ya kazi bali iwe chachu ya utendaji kazi na kutoogopa chochote kilichopo mbele yetu”

Naye Mkuu wa Majeshi Jenerali Venance Mabeyo amesema mbali na wanajeshi 14 waliouawa,kuna mwanajeshi mmoja hajulikani alipo na kwamba wanajeshi wengine 44 ambao ni majeruhi wa tukio hilo wanaendelea na matibabu katika miji ya Kampala, Kinshasa na Goma.
Viongozi wengine waliohudhuria shughuli hiyo ni Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete,Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Afrika Dkt Salim Ahmed Salim,Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Maendeleo ya nchi za Kusini mwa Afrika SADC Dkt. Stagomena Tax,Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa UN na viongozi wa vyama vya siasa,dini na taasisi mbalimbali



MBUNGE MWINGINE WA CHADEMA AJIUZULU

Breaking news

JIFUNZE NAMNA YA KUENDESHA BIASHARA YAKO HAPA KWA HUYU NDUGU.

KAMA UNA NDOTO YA  # KUJIJIRI  AU KUFANYA  # BIASHARA  USIOGOPE ILA JIFUNZE KIDOGO HAPA! Naitwa Andrea. Na nakutana na watu we...